Jumatano , 23rd Sep , 2020

Kutokana na kuadimika kwa biashara ya maua nchini, wadau na wafanyabiashara wa maua jijini Dar es salaam, wameiomba serikali kuhakikisha inasimamia kuanza upya kwa mashamba makubwa ya maua yaliyopo jijini Arusha ambayo kwa sasa hayafanyi uzalishaji.

Maua

"Kiukweli niiombe serikali yangu wayatizame upya yale mashamba ya maua ambayo hayafanyi uzalishaji  hasa kule Arusha na Njombe wawape wawekezaji wenye uwezo wa kuyafufua ili hili soko ambalo leo tunayumba halitakuwepo tena", amesema Angel Rwiza, mfanyabiashara wa maua Namanga Mbuyuni.

Biashara hii ya maua ya asili inadaiwa kushuka zaidi mara baada ya Covid -19 kuathiri zaidi mataifa ya jirani ambayo pia yalikuwa yakiingiza maua hapa nchini mara baada ya kushuka kwa uzalishaji hasa katika mashamba ya ndani.

Aidha biashara hiyo pia imewanufaisha baadhi ya wajasiriamali kwa zaidi ya miaka kadhaa huku wakitoa wito kwa kwa kina mama wengine kujiajiri katika biashara hiyo.

"Nina takribani miaka mitatu kwenye biashara hii ya maua sasa inapotokea Hali Kama hii kwa kweli Hali inatuwia vigumu Sana kwa Sasa kuendesha maisha", Asma Abdallah, mfanyabiashara wa Maua.

Wafanyabiashara wa maua kwa sasa wanatarajia kuwepo kwa mabadiliko mara baada ya kufunguliwa kwa mipaka hasa  kutoka nchi jirani ya Kenya