Friday , 16th Aug , 2024

Uongozi wa timu ya KMC FC ya Jijini Dar es Salaam umeweka malengo ya kumaliza ndani ya nafasi 4 za juu kwenye msimamo wa Ligi Kuu Tanzania Bara 2024-25 iliyoanza kutimua vumbi leo Agosti 16-2024.

Hayo yamezungumzwa na Kocha Mkuu wa KMC FC Abdihamid Moalin ambapo amejivunia usajili bora pamoja na matayarisho kabambe kuelekea msimu mpya na kuweka wazi mipango ya timu hiyo kumaliza kwenye nafasi 4 za juu ndani ya ligi kuu Tanzania Bara 2024-25.

''Usajili wetu umeangalia kila nafasi ambazo zilikuwa na mapungufu katika msimu uliokwisha hivyo naamini wachezaji wangu katika mchezo wetu wa kwanza dhidi Coastal Union wataonyesha kandanda safi na lenye malengo ''amesema kocha Moalin

Kwa upande mwingine,Msemaji wa KMC FC Khalid Chukuchuku amethibitisha kuwa uwanja wao wa KMC Complex uliopo Mwege, jijini Dar es salaam utakuwa unatumiwa na timu tatu za ligi kuu ambazo ni Coastal Union,Simba SC pamoja na wao KMC FC.