Thursday , 15th Aug , 2024

Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) mkoa wa Morogoro imebaini uwepo wa abiria wanaohujumu treni ya umeme (SGR) kwa kulipa nauli ndogo isiyokidhi eneo wanalokwenda

Treni

Naibu Mkuu wa TAKUKURU mkoa wa Morogoro Christopher Mwakajinga, amesema hayo wakati akitoa taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya taasisi hiyo ndani ya miezi mitatu kuanzia mwezi April hadi Juni 2024 na kusema kuwa baadhi ya abiria wanaopaswa kupanda treni hiyo na kushuka katika vutuo vya Pugu, Ruvu na Ngerengere wamekuwa hawatelemki katika vituo hivyo na badala yake hufika hadi Morogoro mjini kwenye stesheni ya Jakaya Kikwete licha ya nauli ndogo waliyolipa

"Uchunguzi uliofanyika umethibitisha kuwa baadhi ya abiria wanaotoka Dar es Salaam hususani wanaolipa nauli za kuishia vituo vya njiani kama vile Pugu kiasi cha sh.1000,Soga sh.4000,Ruvu sh.5000 na Ngerengere 9000 badala ya kushuka katika vituo husika wamekuwa hawashuki na wanaendelea na safari hadi kituo cha mwisho"amesema Mwakajinga Naibu Mkuu wa Takukuru Morogoro.

Aidha katika hatua nyingine amesema taasisi hiyo kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi imefanikiwa kuwafikisha mahakamani dereva, kiongozi wa waendesha daladala na makondakta mkoa wa Morogoro ambao walitaka kumpa rushwa ya shilingi elfu 50  mkuu wa usalama barabarani wilaya ya Mvomero ili awasaidie kusafirisha abiria na magari mabovu.