Friday , 20th Sep , 2019

Wakili wa kujitegemea Fatma Karume amesema amepokea taarifa za kusimamishwa Uwakili Tanzania Bara, na Jaji Kiongozi Eliezer Feleshi, huku mwenyewe akisema hajui sababu iliyomfanya mpaka asimamishwe uwakili Tanzania Bara.

Akizungumza na EATV/EA Radio Digital, Fatma Karume, amesema ameshangazwa na taarifa hizo, kutokana na maamuzi hayo kufanyika bila yeye kuwepo mahakamani na kukosa nafasi ya kujitetea.

"Ni kweli Jaji Feleshi amenipiga 'stop' na wala sijui nini kinafuata kwa sababu mimi sikuwepo mahakamani, na kanipiga stop wala hajaniambia kosa langu ni nini ?'', amesema Fatma Karume.

"Kuhusu hatua zinazofuata mimi sijui nahitaji kutuliza akili yangu, nahitaji kujiuliza na kufikiria kama nahitaji kuendelea kuwa Wakili Tanzania Bara, lakini si lazima niseme sasa hivi nitafanya nini, lakini kwa sasa bado ni mimi ni Wakili Zanzibar." amesema Wakili Fatma Karume

Leo Septemba 20, 2019 Jaji Kiongozi Elinezer Feleshi, ametangaza kumvua uwakili wa Tanzania Bara Fatma Karume, kwa kile alichokieleza anaishambulia ofisi ya Mwanasheria Mkuu.