Friday , 20th Sep , 2019

Mkuu wa Mkoa wa Songwe Brigedia Jenerali Nicodemus Mwangela, amemuagiza Mkuu wa Wilaya ya Momba Juma Irando, kuwaweka rumande baadhi ya watumishi wa Halmashauri walio katika kitengo cha ugavi na ununuzi kwa kushindwa kutoa fedha za ujenzi wa mradi wa soko la mazao la kimataifa.

Mkuu wa Mkoa wa Songwe Brigedia Jenerali Nicodemus Mwangela

Brigedia Mwangela amedai kuwa ni mwaka sasa umepita, tangu Serikali ilipoipatia halmashauri hiyo kiasi cha zaidi ya Shilingi bilioni 8, lakini hadi sasa hakuna kinachoendelea na kwamba yeye hayuko tayari kuona watu wachache wanakwamisha maendeleo.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya hiyo Juma Irando, ameahidi kushughulikia watendaji wote wanaohusika kukwamisha ujenzi wa soko hilo la kisasa, linalojengwa katika kijiji cha Kakozi.

Aidha amemtaka Mkurugenzi wa halmashauri hiyo kujitathimini, kwani ameonekana kuwa kikwazo katika ukamilishaji wa miradi mbalimbali, inayoelekezwa kwake.