Tuesday , 17th Feb , 2015

Chama cha Mpira wa wavu hapa nchini TAVA, kimezitaka timu shiriki za mashindano mbalimbali za mchezo wa mpira wa wavu kuanza maandalizi mapema ili kuweza kuendana na hali ya ushindani wa mchezo huo baina ya nchi moja na nyingine.

Akizungumza na East Africa Radio, Makamu mwenyekiti wa TAVA, Muharame Mchume amesema, katika michuano ya mpira wa wavu wa Ufukweni kanda ya Tano inayoendelea hivi sasa jijini Dar es salaam, kuna ushindani mkubwa kutokana na kila timu kuhitaji ushindi ili kuweza kusonga mbele katika muchuano hiyo.

Mchume amesema, michuano hiyo ilianza kwa timu ya Tanzania wanawake kukutana na Burundi ambapo zilitoka sare na kuingia hatua ya kutafuta seti moja ya ushindi ambapo Tanzania ilishindwa na Burundi hivyo Tanzania kuwa na Pointi saba ikiongozwa na Burundi yenye Pointi nane.

Mchume amesema, kwa muelekeo uliopo kwa timu za Tanzania ambapo ni mara ya kwanza kuandaa michuano hiyo, timu hiyo inauwezo wa kufanya vizuri ambapo kesho timu ya Tanzania itakutana na Kenya na iwapo itaifunga Kenya itakuwa imeweza kuendelea mbele katika mkichuano hiyo.

Mchume amesema, timu zote shiriki za michuano hiyo ambazo ni Kenya, Burundi na wenyeji Tanzania zina uwezo mkubwa unaoonesha kuwa kila timu inahitaji kufanya vizuri ili kuweza kuiweka Afrika katika nafasi nzuri za michezo.