Monday , 21st Nov , 2016

Muingereza Andy Murray ametwaa taji lake la kwanza la ATP World Tour baada ya kumchapa nguli wa mchezo wa tennis duniani Novak Djokovic kwa jumla ya seti 2-0 katika mchezo wa fainali za mashindano hayo.

Andy Murray

Ushindi huo wa 6-3 6-4 katika dimba la O2 Jijini London linalobeba mashabiki 17,000, unamfanya Murray amalize mwaka 2016 akiwa katika nafasi ya kwanza ya viwango vya tennis kwa wanaume duniani.

"Nafurahi sana kwa ubingwa huu, ni muhimu na maalum sana kwangu, ni jambo la kipekee kucheza na Novak Djokovic katika mchezo kama huu" Amesema Murray baada ya kukabidhiwa taji lake.

Raia huyo wa Scottland amesisitiza kuwa licha ya kumaliza mwaka akiwa mchezaji bora lakini, anataka kuendeleza kiwango chake, ili mwaka ujao, aendelee kuwa namba moja.

Kwa ushindi huo, Murray mwenye umri wa miaka 29, ameongeza rekodi yake ya kucheza michezo 24 mfululizo bila kupoteza na kuzima ndoto za Djokovic za kutwaa taji hilo kwa mara ya tano mfululizo.

Djokovic anabaki kuwa na mataji sita ya michuano hiyo sawa na Roger Federer.