Friday , 26th May , 2017

Aliyekuwa mfalme wa muziki wa miondoko ya pwani 'taarab', Mzee Yusuph amewataka watu wote waliokuwa na nyimbo zake kwenye simu wafanye hima kuzifuta kwa madai wakiendelea kuzisikiliza watampatisha dhambi katika hilo.

Mzee Yusuph

Mzee Yusuph amefunguka hayo ikiwa ni masaa machache yamebakia kwa waumini wa dini ya kiislamu kuanza ibada yao ya kufunga mwezi mtukufu wa Ramadhani.

"Mimi nikikubali watu wacheze nyimbo zangu ina maana nimeruhusu dhambi tena ni bora nirudi kuimba muziki tena, hivyo watu wote waliokuwa na nyimbo zangu kwenye simu zao wafute na kuacha kusikiliza ili kuepuka dhambi....Nimetenda sana makosa tena hadharani na kila mtu anajua lakini kwa sasa ninawaomba tu mniombee dua ili niendelee kuwa salama japo hali yangu kiuchumi haiko sawa imebadilika nazidi kupambana ili kipatikane kitu" alisema Mzee Yusuph

Aidha, Mzee Yusuph amesema kwa sasa hajihusishi na masuala ya muziki wa kidunia tena bali ataendelea kuitangaza dini yake pamoja na kuimba nyimbo za kaswida.

Pamoja na hayo, Mzee Yusuph amewasihi waislamu kumrudia Mungu wao kwa kufanya mambo mema katika kipindi hiki cha mfungo pamoja na kuwataka akina baba kuacha manyanyaso kwa wake zao majumbani.