Bi. Hawa - Mama Mzazi wa Chid Benz, alipokuwa akizungumza na eNewz
Akizungumza na East Africa Television, mama wa Chid Benz anayejulikana kwa jina la Bi. Hawa, alisema kwa sasa mtoto wake yuko vizuri, na iwapo ataendelea kupata show na mashabiki kuendelea kumsapoti, atarudi katika hali yake ya kawaida.
“Kwa kweli jinsi nilivyomuona, mashabiki wengi wamekuja kumsapoti Chid Benz, bado hajapoteza mashabiki, tuna imani iwapo kama ataendelea kupata show mara kwa mara na kuweza kupata hizo pesa, atarudi tu, mi najitahidi sana kumuangalia na niko naye karibu sana, na ninapenda kuwataarifu watanzania kwamba Chid Benz yuko vizuri, kwa hiyo naomba mashabiki wake waendelee kmpa sapoti mtoto wangu arudi katika kazi yake”, alisema Bi. Hawa.
Bi. Hawa aliendelea kusema kuwa kwa sasa anamshukuru Mungu kwani Chid Benz ameweza kufanya show ya nguvu na kuwafurahisha mashabiki zake na kusema kuwa amekuwa bega kwa bega katika kumsapoti.
“Nimefurahi sana show ya mwanangu watu wamejaa sana na wanampenda sana, na amejitahidi kuimba nyimbo nyingi sana kwa muda mfupi, mi ni mpenzi sana kutoka kwenye show zake, mara nyingi huwa natoka kwenda kumsapoti mtoto wangu”, alisema Bi. Hawa.
Mwishoni mwa wiki iliyopita kuliandaliwa show maalum kwa ajili ya Chid Benz, show ambayo ilifanya poa baada ya mashabiki kumshangilia wakionesha bado wanamkubali msanii huyo, licha ya anguko alilolipata la kutumia madawa ya kulevya na kumuathiri kwa kiasi kikubwa.