Thursday , 27th Aug , 2015

Familia ya watu tisa imeteketea kwa moto katika tukio la moto ulioteketeza nyumba moja alfajiri ya kuamkia leo eneo la Buguruni Malapa Jijini Dar es Salaam

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Mecky Sadiki

Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Saidi Meck Sadiki amesema watu hao wamefariki wakiwa ndani ya nyumba yao baada ya jitihada zote za kuwaokoa kutoka kwa majirani kushindikana kutoka na moto huo kushamiri.

Aidha Mh. Sadiki amesema ni muhimu kwa kila familia kujitahidi kuwa na mtungi mdogo kwa ajili ya kuzimia moto ili usizidi kupata kasi na kusababisha madhara ambayo yametokea katika familia hiyo ya bwana Mohammed Mathal .

Kwa upande wake Kamishna wa Polisi Kanda maalumu ya Dar es Salaam Suleima Kova amesema kuwa hadi sasa chanzo cha tukio inasemekana ni shoti ya umeme na jiko la gesi lakini polisi wanaendelea na uchuguzi ili kubaini chanzo kamili cha tukio hilo.

Aidha Kamishna Kova amewataka wananchi kuzingatia ushauri wa wajenzi wa makazi katika ujenzi wa nyumba ili kuepuka majanga kama hayo ya moto.

Miili ya marehemu imepelekwa katika hospitali ya Muhimbili kwa ajili ya kuhifadhiwa tayari kwa ajili ya maandalizi ya mazishi ambapo serikali imewapa pole wafiwa na kuahdi kushirikiana na familia hiyo katika shughuli zote za mazishi.