Friday , 3rd Jul , 2015

Serikali imewataka wapima ardhi nchini Tanzania kutotumia nafasi zao katika kujilimbikizia ardhi kwani hali hiyo itaongeza migogoro ya ardhi katika maeneo mbalimbali ya nchi.

Kauli hiyo imetolewa jijini Dar es salaam na Waziri wa Ardhi nyumba na maendeleo ya makazi Mh William Lukuvi katika ufunguzi wa mkutano mkuu wa wataalamu wa upimaji ardhi na utengenezaji wa ramani ambapo amesema kumekuwa na tabia ya baadhi ya wapima adhi kujilimbikizia ardhi na kuziacha bila kujiendeleza na hivyo kusababisha uvamizi wa ardhi kutoka kwa wananchi.

Waziri Lukuvi amesema ili kuboresha mazingira ya wazi ya kiutendaji wataalam wanatakiwa kufuata taratibu zilizoweka katika upimaji wa ardhi na uchoraji wa ramani pia kuzingatia utozaji wa gharama nafuu ambazo zinamwezesha mwananchi wa kawaida kuzimudu.

Kwa upande wake Rais wa taasisi ya wapima ardhi Tanzania (IST) Bw Martin Chodota amesema changamoto kubwa wanayokumbana nayo ni uhusiano usio mzuri baina ya taasisi hiyo na serikali smbso unasababisha kupunguza kasi ya upimaji wa ardhi kuongezeka kwa uhaba wa adhi na migogoro ya ardhi katika maeneo mengi.

Chodota ameongeza kuwa kumekuwa na urasimu katika baraza la wasajili wa ardhi NCPS katika kusajili wapimaji wa ardhi na kutaka baraza hilo kupitia sheria zake ili kutambua mabadiliko ya tekinolojia ili kusaidia wahitimu wapya kusajiliwa na kutambuliwa katika taaluma.