Friday , 20th May , 2016

Wanafunzi wa shule ya sekondari ya Mustafa Sabodo iliyopo halmashauri ya wilaya ya Mtwara, wako hatarini kupata magonjwa ya milipuko pamoja na kung’atwa na wadudu kutokana na kujisaidia maporini.

Wanafunzi wakiangalia vyoo wanavyotumia (Picha na Maktaba)

Wakizungumza shuleni hapo, wanafunzi hao wamesema tatizo hilo ni la muda mrefu na kwamba linatokana na kukosekana kwa vyoo karibu na mabweni ambapo wanalazimika kutembea umbali mrefu kwa ajili ya kwenda kujisaidia huku baadhi yao wakiamua kujisaidia katika mapori yaliyopo nyuma ya mabweni yao.

Mwalimu Mkomo Katani, ambaye husimamia masuala ya afya za wanafunzi shuleni hapo, ameiomba serikali kuushinikiza uongozi wa shule kuona umuhimu wa kujenga vyoo karibu na mabweni ili kuhepusha athari za kiusalama kwa wanafunzi pamoja na kupatwa na magonjwa ya milipuko.

Mkuu wa mkoa wa Mtwara, Halima Dendego, ambae amefika shuleni hapo kusikiliza kero mbalimbali pamoja na kupokea maoni ya walimu ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kutembelea sehemu mbalimbali mkoani humo, ameutaka uongozi wa shule kushirikiana na jamii inayowazunguka kutatua changamoto hizo ambazo zipo ndani ya uwezo wao.