Saturday , 17th May , 2014

Katibu mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA Dkt Wilbroad Slaa amesema Umoja wa Katiba ya Wananchi UKAWA kamwe haitasambaratika kwa sababu ya kupigania madaraka.

Dkt Wilbroad Slaa akihutubia umati wa wananchi  mjini Arusha

Dkt Wilbroad Slaa amesema UKAWA hawatakimbilia kugawana madaraka badala yake watapambana  kupigania kuona wananchi wanapata katiba  mpya itakayowakomboa.
 
Dkt Slaa ameyasema hayo wakati akihutubia umati wa wananchi  mjini Arusha wakati wa mkutano wa  kuelimisha wananchi juu ya umuhimu wa katiba ambapo amesema ukawa  siku zote unapigania ukombozi wa taifa  hili  ili kuhakikisha  wananchi wanapata katiba  itakayotoa  majibu ya kero za  wananchi.

Naye mbunge wa jimbo la Moshi mjini Mh Philemon Ndesamburo  amewahakikishia wananchi kuwa UKAWA utazunguka nchi nzima kuwaeleza wananchi ukweli  juu  katiba inayowasaidia  kujikomboa katika umasikini.
 
Huko mkoani Iringa mamia ya wananchi wa wilaya ya Mufindi wamejitokeza kwa wingi katika mkutano wa  UKAWA.

Akizungumza na wananchi hao  mwenyekiti wa chama cha wananchi CUF Prof Ibrahimu Lipumba amewataka wananchi wa Mufindi mkoani Iringa  kuendelea kuunga mkono Umoja wa Katiba ya Wananchi UKAWA ili watanzania wapate katiba itakayoweza kuhakikisha rasilimali za nchi zinawanufaisha wananchi wenyewe na si kunufaisha wachache na kuwaacha wengine wakiendelea kuteseka kwa hali ngumu za maisha na kukosa huduma muhimu zikiwemo za afya na elimu.