Tuesday , 17th Feb , 2015

Taasisi ya Afrika ya Sheria za Kimataifa (AIIL) itakayofundisha Waafrika Elimu na Utaalamu wa Sheria za Kimataifa na hivyo kupunguza utegemezi wa wataalam kutoka nje, hususan, katika kuingia mikataba na wawekezaji wa nje, imezinduliwa jijini Arusha.

Makamu Rais wa Mahakama ya Kimataifa ya Haki (ICJ) na Rais wa Bodi ya AIIL, Jaji Abdulqawi Yusuf.

.Kuzinduliwa kwa Taasisi hiyo yenye makao yake makuu Jijini humo kunatajwa kuwa hatua muhimu katika kuongeza hadhi ya Jiji hilo kuwa na mwonekano wa The Hague kutokana na kusheheni mahakama nyingi za kimataifa.

Makamu wa Rais wa Mahakama ya Kimataifa ya Haki (ICJ) na Rais wa Bodi ya AIIL, Jaji Abdulqawi Yusuf, akizungumza Jijini Arusha wakati wa kuzinduliwa kwa Taasisi hiyo amesema kwa muda mrefu Afrika imeonekana kuwekwa kando katika usukani wa masuala ya Sheria ya Kimataifa lakini kwa kuazishwa kwa taasisi hiyo kunafungua ukurasa wa kuiletea Afrika sifa nyingine katika kada ya Sheria.

Akizindua taasisi hiyo jijini hapa, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Dk. Mahadhi Juma Maalim,amesema Tanzania itatoa msaada kuhakikisha taasisi hiyo inafanya shughuli zake kwa malengo iliyojiwekea huku akibainisha kuwa hakuna shaka kwamba taasisi hiyo itatoa mchango mkubwa katika kupunguza tatizo la rasilimali watu.

Kwa upande wake, Mhadhiri Mwandamizi na Sheria kutoka Chuo Kikuu cha Zanzibar Profesa Chris Peter Maina, ambaye ni mjumbe wa Tume ya Sheria za Kimataifa, akiwasilisha mada kuhusu changamoto za uwekezaji wa nje katika nchi za Afrika, amesem taasisi hiyo imeanzishwa wakati muafaka akitolea mfano katika miaka ya 1960 ambapo Tanzania ilikuwa na viongozi waadilifu ingawa hapakuwa na wataalamu wengi tofauti na sasa ambapo kunaripotiwa uingiaji wa mikataba mibovu inayoligharimu taifa licha ya uwepo wa utitiri wa wataalamu.

Pamoja na masuala ya utafiti wa kisheria, taasisi hiyo inatarajiwa kutoa mafunzo ya muda mfupi, stashahada ya uzamili, shahada ya uzamili na uzamivu katika sheria za kimtaifa.