Thursday , 8th Dec , 2016

Wafugaji wa  jamii ya kimasai walioko katika kijiji cha Kambala wamesema mgogoro uliopo baina yao na wakulima  wa  vijiji jirani kwa kiasi kikubwa unachochewa na baadhi ya wakulima wanaotoka katika Manispaa ya Morogoro.

Mfereji mkubwa wa kutenganisha eneo la wafugaji wa kijiji cha Kambala na wakulima wa bonde la Mgongola wilayani Mvomero

 

Wakitoa madai hayo mbele ya mkuu wa  wilaya ya Mvomero Muhammed Utaly, wafugaji hao wamedai kuwa wanatambua mchango mkubwa toka kwa wakulima na hapo awali walikuwa wakiishi kama ndugu lakini mara baada ya wakulima toka manispaa kuingia katika eneo hilo ndiyo chanzo cha mgogoro kuanza.

Mkuu wa wilaya amewata wafugaji hao kuwa makini  na watu wanaojiita wapiga dili ambao ndiyo chanzo cha  kuwapo kwa mgogoro baina ya wakulima na wafugaji.

Katika hatua nyingine mwenyekiti wa kijiji hicho amemuhakikishia mkuu huyo wa wilaya kuwa wafugaji wote wamechoshwa na migogoro hiyo, hivyo kwa sasa wamepanga kwenda kutoa kesi iliyoko mahakamani ili suala hilo limalizwe nje ya mahakama.

Pia wamemuomba mkuu wa wilaya kusimamia mazungumzo hayo ili kumaliza mgogoro huo wa wakulima na wafugaji.