Friday , 6th May , 2016

Serikali imesema imeanza kutafuta njia sahihi ya kuondoa Migogoro ya Ardhi ambayo mingi imetokana na kuongezeka kwa matumizi ya ardhi, pamoja na kuongezeka kwa mifugo pamoja na utendaji mbovu wa watendaji wa maeneo hayo.

Waziri Mkuu wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa

Akizungumza bungeni Jijini Dodoma, Waziri Mkuu wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa, amesema tayari wameshaanza kuunda timu maalumu kwa kuunganisha wizara tatu zenye dhamana ambazo ni Wizara ya Ardhi, Wizara ya Maliasili pamoja na Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi.

Mhe. Majaliwa amesema kuwa wizara hizo zimetakiwa kuweka mipaka mipya ikiwa ni pamoja na kuongeza maeneo ya ufugaji ikiwa ni sambamba na kutumia ranchi za taifa kwa wafugaji wa kawaida na wafugaji wakubwa.

Katika hatua nyingine Waziri Majaliwa amesema kuwa atafanya ziara katika mikoa tofauti akianza na Mkoa wa Tabora ambapo pamoja na mambo mengine ataenda kuangalia migogoro ya ardhi katika eneo hilo na Changamoto inayowakuta wakulima wa zao la Tumbaku.

Mhe Majaliwa amesema serikali ya Awamu ya Tano imedhamiria kuwafanya wakulima, na wafugaji waone tija ya mifugo au Kilimo chao kwa kuweza kupata masoko hata nje ya nchi.