Monday , 19th May , 2014

Mgomo wa wafanyakazi wa Shirika la Reli la Tanzania na Zambia (TAZARA), umeendelea leo licha ya Serikali kuahidi kutatua madai yao ikiwa ni pamoja na malipo ya mshahara yao ya kuanzia mwezi wa Februari hadi Aprili.

Mapema leo East Africa Radio imeshuhudia wafanyakazi wa Shirika hilo wakiwa wamekusanyika nje ya jengo la shirika hilo, huku wakisisitiza kutorudi kazini hadi mishahara ya miezi yote wanayodai itakapolipwa pamoja na kuhakikishiwa tatizo hilo kutojirudia tena.

Mmoja wa wafanyakazi wa TAZARA ameeleza kuwa wameletewa taarifa kutoka kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi kupitia Katibu Mkuu wa TRAWU Erasto Kiwele zinazoelezea kuwa serikali ya Tanzania imekubali kutoa mshahara wa mwezi Februari na Aprili huku serikali ya Zambia ikishughulikia mshahara wa mwezi Machi na Mei.

Mgomo wa wafanyakazi wa TAZARA ulianza Mei 12 kwa madai ya kutolipwa mishahara ya kuanzia mwezi Februari hadi Aprili mwaka huu.