Thursday , 28th May , 2015

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Chiku Gallawa ameziagiza shule zote za msingi na sekondari mkoani hapa kuwa na mashamba darasa ya zao la mtama ili wananfunzi wawe na uhakika wa chakula mashuleni.

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Chiku Gallawa akiwaelezea wananchi wa kijiji cha Damai Kondoa malengo ya kuzindua msimu wa kilimo mwaka 2015 Mkoani Dodoma

Gallawa ametoa agizo hilo jana Wilayani Chamwino Mkoani Dodoma wakati akizindua majengo ya shule ya msingi Suli ambayo imejengwa upya na shirika la Majirani wema kutoka nchini Korea Kusini baada ya majengo ya awali kuchakaa.

Amesema kuwa Mkoa wa Dodoma una asilimia 56 ya udumavu wa akili hivyo kwa kula nafaka kama za mtama pamoja na virutubisho vingine kutasababisha watoto watakazozaliwa kuwa na afya bora tangu tumboni.

Aidha amewaagiza wanaume wa Mkoa wa Dodoma kuuza rasilimali walizonazo kwa ajili ya kununua chakula cha akiba katika familia zao kwani mwaka huu mvua hazikunyesha za kutosha hivyo kuna uwezekano mkubwa wa kuwa na njaa.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Shirika la Mpango wa Chakula Duniani Mkoa wa Dodoma (WFP), Neema Sitta amesema kuwa Shirika hilo litatoa chakula kwa wanafunzi wa shule hiyo ili kuwafanya watoto kuwa na utulivu wakati wa masomo.