Saturday , 26th Jul , 2014

Kamati ya Mashauriano ya Bunge Maalumu la Katiba nchini Tanzania imependekeza kuendelea kwa vikao vya Bunge hilo Agosti 5 mwaka huu hata kama wajumbe wa kundi la umoja wa Katiba ya Wanainchi UKAWA wataendelea kususia vikao hivyo.

Bunge la Katiba Tanzania

Taarifa iliyotolewa jijini Dar es salaam jana na Katibu wa Bunge hilo Bw. Yahaya Hamad kwa niaba ya mwenyekiti wa bunge hilo Samuel Sitta amesema kamati hiyo ilikutana Julai 24 mwaka huu na katika kikao hicho wajumbe walijadili matatizo yaliyojitokeza katika vikao vya Bunge lilipopita na kupendekeza Bunge hilo liendelee na vikao vyake.

Katibu wa Bunge la Katiba amesema jitihada mbali mbalizilifanywa na Sekretarieti pamoja na Mwenyekiti wa Bunge kuwashawishi wajumbe wanaounda umoja wa UKAWA kutoka vyama vya CUF, CHADEMA na NCCR Mageuzi kurudi bungeni lakini hazikuzaa matunda.

Bw. Hamad amesema kuna athari kubwa za kutoendelea na mchakato huo na baadaye kupigiwa kura za maoni kwani mabilioni ya fedha za wananchi yametumika katka kazi hiyo na baya zaidi kuiweka rehani amani ya nchi kwa kuukuza mgogoro wa katiba, kuwagawa wananchi kwa propaganda hadi Uchaguzi mkuu wa mwaka 2015.