Ijumaa , 25th Mei , 2018

Yakiwa yamebakia masaa machache kuelekea mechi ya Yanga SC dhidi ya Ruvu Shooting hii leo, Afisa Habari wa wanajangwani Dismas Ten amesema watatumia mchezo huo kujipatia matokeo mazuri ili wajiweke imara kwenye kinyang'anyiro cha mshindi wa nafasi ya pili Ligi Kuu.

Dismas amebainisha hayo wakati alipokuwa anaelezea maandalizi yaliyofikiwa mpaka hivi sasa na kikosi chake kuelekea kupambana na Ruvu Shooting ambapo kila mmoja amempania mwenzake kumuangamiza ili apata kukaa sehemu yenye utulivu licha ya Ligi kuwa ndio inaelekea ukingoni kwa msimu huu wa mwaka 2017/18. 

"Ni mchezo mgumu kwa sababu Ruvu Shooting wamekuwa wanapata matokeo mazuri kwenye michezo yao kadhaa iliyopita kwa hiyo huwezi kubedha unaenda kucheza na timu ya aina gani lakini mwisho wa siku nini tunahitaji hilo ni suala jingine", amesema Dismas.

Pamoja na hayo, Dismas ameendelea kwa kusema "tunahitaji kupata matokeo kwenye michezo yote iliyobaki lengo letu ni kuona tunashika nafasi ya pili kwasababu bingwa tayari ameshapatikana na sisi tunahitaji kulinda heshima ya klabu na timu yetu kwa hiyo tunahitaji kushinda mchezo wa leo ili tujiweke sawa katika nafasi ya pili".

Kwa upande mwingine, Dismas Ten amesema hali ya wachezaji kiujumla ipo vizuri na daktari amewathibitishia hilo ila kuhusu nani na nani atakuwepo sehemu la mchezo jukumu hilo wameliachia benchi la ufundi.