Alhamisi , 24th Mei , 2018

Mshambuliaji wa kimataifa wa Tanzania Thomas Ulimwengu, amerejea barani Afrika na sasa atajiunga na klabu ya Al Hilal ya nchini Sudani.

Ulimwengu aliyewahi kucheza TP Mazembe kwa mafanikio makubwa akifanikiwa kutwaa mataji mbalimbali likiwemo la Klabu bingwa Afrika, anarejea Afrika baada ya kuachana na klabu ya AFC Eskilstuna iliyokuwa ikishiriki Ligi kuu nchini Sweden kabla ya kushuka daraja msimu uliopita.

Mshambuliaji huyo, anatazamiwa kutua katika klabu hiyo ya Al hilal na taarifa za awali zinaeleza kuwa atasaini mkataba wa miaka miwili kukitumikia kikosi hicho.

Hapo awali aliwahi kucheza na mtanzania mwenzake Mbwana Samatta katika klabu ya TP Mazembe na kwa sasa pacha wake huyo anahudumu katika kikosi cha KRC Genk ya nchini Ubelgiji.