Jumatano , 16th Mei , 2018

Kuelekea mchezo wa leo wa Kombe la shirikisho barani Afrika hatua ya makundi kati ya wenyeji Yanga dhidi ya Rayon Sports ya Rwanda, kocha msaidizi wa Simba Masoud Djuma na kiungo Haruna Niyonzima wameitembelea Rayon kambini.

Wawili hao wameitemebelea kambi ya Rayon Sports, huku wakiacha maswali mengi kwa mashabiki wa soka nchini wengi wakiamini kuwa wamepeleka mbinu za namna ya kucheza na Yanga kwasababu wao wanaifahamau vizuri Yanga ya msimu huu.

Haruna Niyonzima ambaye ni raia wa Rwanda amewahi kuwa mchezaji wa Rayon Sports kati ya miaka ya 2006 - 2007 kabla ya kujiunga na APR na baadae Yanga ambayo aliichezea hadi msimu uliopita hivyo ameitembelea klabu yake ya zamani.

Kwa upande wake kocha Masoud Djuma naye ameitembelea klabu yake hiyo ya zamani ambayo msimu uliopita kabla ya kutua Simba ndiye alikuwa kocha mkuu wa Rayon Sports na aliipa ubingwa wa Rwanda.

Mchezo huo utapigwa usiku kuanzia saa 1:00, kwenye uwanja wa taifa jijini Dar es salaa. Yanga inashika mkia ikiwa haina alama huku Rayon Sports inashika nafasi ya tatu ikiwa na alama 1 kwenye kundi D linaloongozwa na U.S.M Alger yenye alama 3 na Gor Mahia alama 1.