Jumanne , 11th Mei , 2021

Klabu kongwe na watani wa jadi nchini Simba na Yanga zimejua hatma zao kwenye michuano ya kombe la shirikisho (Azam sports federation Cup ) watacheza dhidi ya timu gani kwenye hatua ya robo fainali, baada ya droo ya michezo ya hatua hiyo kufanyika hii leo.

Wachezaji wa Simba na Yanga wakiwania mpira kwenye moja ya mchezo wa ligi kuu Tanznaia bara

Droo ya michezo ya hatua hiyo imefanyika leo asubuhi ambapo jumla ya timu nane (8) ndizo zilizohusika kwenye droo hiyo timu saba ni za ligi kuu ambazo ni Simba SC, Yanga SC, Azam FC, Mwadui FC, Dodoma jiji, Biashara United, Namungo FC na timu moja ya daraja la kwanza ambayo ni Rhino Rangers.

Mara baada ya droo hiyo kuchezeshwa mabingwa watetezi wa michuano hii Simba SC wataminjyana na Dodoma jiji mchezo ambao Simba watakuwa wenyeji, Klabu ya Yanga watakuwa ugenini na watacheza dhidi ya Mwadui FC, Rhino Rangers watakuwa wenyeji wa Azam FC, na mchezo mwingine Biashara United watakuwa wenyeji wa Namungo FC.

Ratiba michezo ya robo fainali

Katika hatua ya nusu fainali nusu fainali ya kwanza itakuwa kati ya mshindi wa jumla wa mchezo kati ya Simba dhidi ya Dodoma atacheza na mshindi wa mchezo kati ya Rhino Rangers na Azam FC, na nusu fainali ya pili itakuwa kati ya mshindi wa jumla wa mchezo kati ya Biashara United dhidi ya Namungo na mshindi wa mchezo kati ya Mwadui dhidi ya Yanga.

Na michezo ya nusu fainali msimu huu itachezwa katika mikoa miwili tofauti, mchezo mmoja utachezwa Songea Ruvuma na mchezo mwingine utachezwa Mkoani Tanbora wakati mchezo wa fainali utapigwa katika dimba la Lake Tanganyika Kigoma.