Jumatano , 23rd Mei , 2018

Nahodha wa timu ya soka ya Tanzania, Taifa Stars Mbwana Ally Samatta ameingia kwenye vita ya kimichezo na msanii Alikiba inayotarajiwa kufanyika Juni 9, 2018 katika dimba la Taifa Jijini Dar es Salaam kwa lengo la kuhamasisha uchangiaji wa vifaa na miundombinu mashuleni.

Akizungumzia mpambano huo Samatta amesema mechi hiyo itakuwa itamuhusisha yeye na rafiki zake wanaomkubali  dhidi ya Alikiba akiwa na rafiki zake pia.

"Ni mechi ya hisani ya Samatta 11 na AliKiba 11, nitachagua rafiki zangu na Ali atachagua rafiki zake. Hii ni mechi ya hisani kama zilizo nyingine ambazo zimekuwa zikifanywa na wachezaji wakubwa, nataka nifanye moja lakini itakuwa na radha tofauti, kwani timu pinzani itakuwa ya AliKiba", amesema Samatta.

Kwa upande wake AliKiba amesema amefurahi urafiki wake na Samatta kuzalisha kitu hicho kizuri huku akiwaomba wapenzi na mashabiki wake kujitokeza kwa wingi uwanja wa Taifa Juni 9 kwenye mchezo huo wa Hisani.

Mgeni rasmi siku hiyo anatarajiwa kuwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Harrison George Mwakyembe.