Jumamosi , 15th Jul , 2017

Real Madrid inajiandaa kupeleka ofa nyingine Manchester United kwa ajili ya kumsajili golikipa wa timu hiyo, David de Gea.

David de Gea

United wanataka kumbakisha golikipa huyo lakini itakuwa tayari kumuachia kwa dau la pauni milioni 60, fedha zitakazomfanya De Gea kuweka rekodi ya Dunia kwa uhamisho wa magolikipa.

Real Madrid wamepania kuona golikipa huyo wa zamani wa Atletico Madrid anatua jijini Madrid kuitumikia timu hiyo baada ya kumkosa mwaka 2015.

Awali United iliweka wazi kutokuwa tayari kumuuza golikipa huyo, lakini dau la Real Madrid ni wazi litawafanya wababe hao wa England kumuachia golikipa huyo aliyedumu Old Trafford kwa miaka sita sasa.

De Gea alikaribia kutua Real Madrid mwaka 2015 lakini uhamisho huo ulikwama dakika za mwisho na kwa sasa tayari ameonyesha nia ya kweli ya kutaka kujiunga na mabingwa hao wa Ulaya.

Golikipa huyo ameonekana kutokuwa na wakati mzuri ndani ya Manchester United chini ya kocha Jose Mourinho ukilinganisha na wakati wa utawala wa kocha Louis van Gaal na kwa sasa anataka kurejea nchini kwao.

United ilimsajili De Gea mwaka 2011 akitokea Atletico Madrid kwa ada ya pauni milioni 18.9 na kuwa muhimili mkubwa wa timu hiyo.