Ijumaa , 25th Mei , 2018

Nyota wa Tanzania  Simon Msuva anayekipiga kwenye klabu ya Difaâ Hassani El Jadidi ya ligi kuu ya Morocco, amekubali kuchezea timu ya Marafiki wa Mbwana Samatta katika mechi maalum ya hisani.

Msuva amethibitisha hilo kwa kusema atatua nchini tayari kuchezea timu ya nyota huyo mwenzake anayekipiga Ubeligji dhidi ya timu ya msanii Ali Kiba na rafiki zake ambapo mechi hiyo ni maalum kwa  kuhamasisha uchangiaji wa vifaa na miundombinu mashuleni Juni 9.

''Nitakuwepo uwanja wa taifa jijini Dar es salaam hiyo Juni 9 mwaka huu na nitachezea timu ya ndugu yangu Samatta ili kuwasaidia wanafunzi wetu kupata vifaa na hatimaye wakapate elimu bora kwa faida ya taifa letu kwa siku zijazo'', amesema.

Mechi hiyo inawakutanisha wachezaji ambao ni marafiki wa Samatta anayechezea KRC Genk ya Ubeligiji na timu ya marafiki wa msanii Alikiba ambaye naye anasifika kwa kusakata soka.