Ijumaa , 25th Mei , 2018

Hofu ya usalama katika mji wa Kiev nchini Ukraine, imeongezeka baada ya mashabiki wawili wa timu ya Liverpool kushambuliwa na genge la wahuni ikiwa imebaki siku moja kabla ya mchezo wa fainali wa mashindano ya klabu bingwa Ulaya.

Gazeti la Independent limeandika kuwa, Polisi nchini Ukraine, wamethibitisha tukio hilo na kudai kuwa wa mashabiki wawili wa Liverpool wamejuruhiwa katika ya mji wa Kiev mahali ambapo kundi la mashabiki hao walikuwa wamewasili katika mgahawa wa Rooster Grill.

Polisi wameongeza kuwa watu wawili wanashikiliwa kufuatia tukio hilo ingawa wengi wao walifanikiwa kukimbia katika eneo la tukio. Mmoja wa mshabiki Liverpool, Jason Frost amethibitisha kushambuliwa masaa mchache baada ya kuwasili katika mji huo 

“Tulikuwepo hapa kwa masaa manne  na kisha baadae tukaanza kushambuliwa, walikuja  kama kundi la mbwa, ilikuwa inaogopesha sana, tulikuwa tunapata chakula cha jioni, sikuja hapa kwa mambo haya, bali nilikuja kuangalia mpira” amesema Bwana Frost.

Kesho Mei 26, timu ya Liverpool kutoka England itakabiliana na Real Madrid ya Hispania katika mchezo wa mashindano ya klabu bingwa Ulaya utakaofanyika mjini Kiev katika nchi ya Ukraine.