Jumatano , 16th Mei , 2018

Timu ya Lipuli FC inatarajiwa kushuka katika dimba la Manungu Turiani Mkoani Morogoro kuvaana na Mtibwa Sugar huku ikiwa inawakosa nyota wake sita kutokana na sababu mbalimbali zilizokuwa nje ya uwezo wao.

Hayo yamebainishwa na Kocha wa Lipuli, Seleman Matola wakati akizungumzia maandalizi ya mwisho ya kikosi chake kinachoenda kutafuta alama tatu mbele ya Mtibwa Sugar kwenye muendelezo wa kumaliza michuano ya Ligi Kuu Tanzania Bara kwa msimu wa mwaka 2017/18 na kuwataja nyota hao kuwa ni Jamali Mnyate, Stephen Mganga, Golikipa Yusuf, Fred Tangaru, Omega pamoja na Emmanuel Kichiba. 

"Tunaendelea vizuri maandalizi yetu dhidi ya Mtibwa Sugar japo nina amini mechi hii itakuwa ngumu sana kwa sababu Mtibwa ni miongoni mwa timu ngumu katika ligi kuu. Katika mchezo wa leo tutawakosa baadhi ya wachezaji kutokana na kuwa majeruhi wengine wana kadi za njano pamoja na kuwepo na matatizo ya kifamilia", amesema Matola.

Aidha, Matola amesema japokuwa timu yake itawakosa wachezaji hao lakini imejipanga vizuri kuhakikisha wanapata matokeo mazuri katika mchezo huo ili iweze kujiweka vizuri kwenye msimamo wa ligi.

Lipuli FC kwa sasa inashikilia nafasi ya 8 kibindoni ikiwa na alama 32 kwa michezo 27 huku Mtibwa Sugar yenyewe ikishika nafasi ya 6 kwa alama 37 yenyewe ikiwa imecheza michezo 27.