Ijumaa , 25th Mei , 2018

Nahodha wa Klabu ya Mabingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara msimu wa mwaka 2017/18 na mshambuliaji wa Simba, John Bocco amefunguka na kudai watahakikisha katika mchezo wao ujao dhidi ya Majimaji FC wafanye vizuri zaidi ili waweze kujenga heshima yao waliyoikusudia kuifanya.

Bocco ametoa kauli hiyo wakati akizungumza na mwandishi wa habari hii na kusema wanajua mchezo huo utakuwa mgumu sana kwa upande wao kutokana na wapinzani wao Majimaji wanapambana ili kujinusuru kutoshuka daraja.

"Tunakubali tumepoteza na tunaacha matokeo ya mchezo uliopita tunachoangalia sasa hivi ni mchezo uliokuwa mbele yetu dhidi ya MajiMaji, ni mechi itakuwa ngumu sana kwasababu wapinzani wetu wapo katika hatari ya kushuka daraja", amesema Bocco.

Pamoja na hayo, Bocco ameendelea kwa kusema "kwa hiyo watajitahidi ili wasiweze kushuka na sisi pia tupo katika kujenga heshima yetu ambayo tuliteleza katika mchezo uliopita".

Simba SC inashuka dimbani Mei 28, 2018 mkoani Songea kuvaana na Majimaji huku ikiwa na alama 68 ikishikilia kilele ya ligi kuu kwa michezo 29, Majimaji yenyewe ikishika nafasi 15 kwa alama 24 ikicheza jumla ya michezo 29.