Alhamisi , 12th Oct , 2017

Msanii wa muziki wa Injili, Emanuel Mbasha ambaye wengi humsifia kwa utanashati wake, amesema anamshukuru Mungu kwa kuonyeshwa kupendwa, baada ya mabinti wengi kumtamani kimapenzi.

Akiongea na eNewz ya East Africa Television, Emmanuel Mbasha amesema ingawa wanawake wengi wanafunguka hisia za mapenzi juu yake, lakini anamuomba Mungu ampe mtu sahihi zaidi ili yasije yakajirudia yaliyomkuta awali.

"Wadada wengi wananipenda wa kila aina na hiyo iko wazi, ukiangalia DM yangu kila siku inajaa meseji, kuna kila aina, na ninamshukuru Mungu kwa kipaji hicho, maana yake kupendwa nako ni kibali na ni baraka za Mungu, sasa nikikurupuka tu kuchukua nitaingia majanga, natamani nipate mtu sahihi, nifanye naye maisha tupate watoto tuendelee mbele, maana yake sitawaza kukaa hivi milele ila kwa sasa sina sababu ya kukurupuka", amesema Emmanuel Mbasha.

Mbasaha ambaye amesema amechoshwa na  upweke, ameendelea kusema kwamba..."mimi nimetokea kwenye changamoto kubwa sana ya mahusiano, angekuwa mwengine angedata angeanza kunywa pombe, kuvuta bangi na kufanya mabaya, lakini nilisimama na Mungu, hivyo nimetulia nikisubiria Mungu aniletee mtu sahihi".

Emmanuel Mbasha ameachana na aliyekuwa mke wake ambaye pia ni mwanamuziki wa nyimbo za Injili, Flora Mbasha, huku akimshtaki kwa kosa la kumbaka mdogo yake, kesi ambayo Emmanuel aliachwa huru kutokana na kukutwa hana hatia.