Jumatano , 9th Jun , 2021

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amewataka wakurugenzi wa Halmashauri zote nchini kuhakikisha wanafufua madarasa kwa ajili ya Mpango wa Elimu ya Msingi kwa walioikosa (MEMKWA) ili kusaidia kupunguza ongezeko la watu wazima wasiojua kusoma na kuandika.

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa

Waziri Mkuu ametoa agizo hilo leo, Juni 9, 2021 wakati wa ufunguzi wa Kongamano la Kimataifa la Kuadhimisha Miaka 50 ya Elimu ya Watu Wazima Tanzania ambapo amesema suala la kuhuisha elimu ya watu wazima limekuja wakati muafaka hapa nchini kwani nchi yetu tumeshaingia katika uchumi wa taifa la kati.

“Naagiza madarasa ya MEMKWA yahuishwe, wakuu wa mikoa na wilaya suala la elimu ya watu wazima liwe sehemu ya ajenda zenu mnapofanya ziara, Fuatilieni kuiona elimu ya watu wazima inahuishwa ili kupunguza na ikiwezekana kuondoa kabisa tatizo la kutokujua kusoma na kuandika” amesema Waziri Mkuu

Pia amewataka watumie madarasa hayo kuwezesha watu wazima wapate stadi mbalimbali pamoja na stadi za Kusoma, Kuandika na Kuhesabu (KKK)

Aidha Majaliwa amesema kuwa pamoja na kutekeleza majukumu mengine, Taasisi ya Elimu ya Watu wa Wazima iendelee kutekeleza kikamilifu jukumu lake la msingi la utoaji wa elimu ya watu wazima hadi katika ngazi ya wilaya

“Andaeni mkakati wa kusimamia utoaji mafunzo ya stadi za Kusoma, Kuandika na Kuhesabu (KKK) kwa watu wazima badala ya kutoa astashahada, shahada na stashada tu. Idadi wa Watu wazima wasiojua kusoma imeongezeka hamna jinsi ya kukwepa jukumu lenu hili, Jipangeni upya ninafahamu fika Elimu ya Watu Wazima ni zaidi ya KKK” amesema Waziri Majaliwa

Sambamba na hilo, Majaliwa amewataka wataalam na wanataaluma wa elimu ya watu wazima kutoa ushauri kuhusu namna ya kuboresha vyuo vya kati vinavyotoa mafunzo mbalimbali ili kuzalisha wahitimu mahiri wanaohitajika katika viwanda na taasisi nyingine.