Jumanne , 10th Jan , 2017

Baadhi ya wakulima wa kata ya Chitego wilaya ya Kongwa mkoani Dodoma, wameandamana hadi ofisi za halmashauri ya wilaya hiyo kulalamikia kuibuka upya kwa mgogoro kati yao na wafugaji.

Mkutano wa wananchi wa kijiji cha Kongwa wilayani Kongwa baada ya kutokea vurugu za wakulima na wafugaji (Picha: maktaba)

Akizungumza kwa niaba ya wenzake jana, mkulima Daudi Chitila, amesema kutokana na kuibuka kwa mgogoro wa mara kwa mara, wanaomba eneo hilo kupimwa ili kuondokana na migogoro hiyo kati yao na wafugaji.

Chitila amesema migogoro hiyo imekuwa ikijitokeza hasa wakati wa kipindi cha kilimo kinapoanza kutokana na wafugaji wengi kuachia makundi ya mifugo yao hasa ng’ombe kuingia mashambani.

“Tunawaomba viongozi wa wilaya mliopo hapa kusikiliza kilio chetu cha muda mrefu, njooni mpime maeneo hayo na kuanisha matumizi ya kilimo na ufugaji ili kuondoa mgogoro huu,” amesema Chitila.

Hali ilivyowahi kuwa baada ya vurugu za wakulima na wafugaji wilayani Kongwa

Katika mgogoro huo ulioanza hivi karibuni, baadhi ya wakulima wamejeruhiwa na wafugaji kutokana na kugombea maeneo ya malisho na kilimo, jambo ambalo lisipodhibitiwa mapema linaweza kuhatarisha uvunjifu wa amani.

Mwenyekiti wa halmashauri ya Kongwa, White Zuberi, amewataka wakulima hao wawe wavumilivu na kutolipiza kisasi kwa wenzao wafugaji.

Hata hivyo, amewaagiza watendaji wa kata na vijiji zote wilayani hapo kuhakikisha wanatenda haki katika kusimamia sheria za ardhi.

Mgogoro huo wa ardhi katika eneo hilo ulikuwa ukiibuka mara kwa mara hasa msimu wa kilimo unapoanza hususani katika vijiji vya Chitego, Lenga na Wali ambacho kimeingia wilaya mbili za Chamwino na Kongwa.