Ijumaa , 1st Jul , 2022

Ofisi ya Waziri Mkuu-kazi Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu imeanza kugawa vifaa Mtaji kwa vikundi vya vijana 175 vyenye jumla wa vijana 1,741 watakaopatiwa vifaa hivyo ikiwa wanatoka katika Mikoa yote 26 Tanzania Bara na Vyuo 3 vya Watu Wenye Ulemavu ambavyo vinasimamiwa na Ofisi hiyo.

Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira,na Wenye ulemavu, Patrobas Katambi amekabidhi vifaa hivyo tarehe 01 Julai, 2022 jijini Dodoma ambavyo ni; Vyerehani 400; Seti 75 za Mashine za uchomeleaji na Uungaji vyuma pamoja na seti 70 za mashine za kutengeneza vifaa vya Aluminiam vikiwa na thamani ya Shilingi milioni 371,075, 296.

“Nimshukuru Mhe.Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuwawezesha vijana ili waweze kujiajiri. Tunawashukuru wadau ambao wamekuwa wakishirikiana na Serikali katika kuwezesha vijana kujiajiri hususan Shirika la Kazi Duniani (ILO). ILO wametoa mchango mkubwa katika kuwezesha upatikanaji wa vifaa mtaji”

Katambi amekabidhi vifaa mtaji kwa Ofisi ya Rais-TAMISEMI kwa kuwa Ofisi hiyo, inatekeleza mipango ya kuwezesha vijana kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais-TAMISEMI kwakuwa TAMISEMI huwaratibu vijana ambao ndiyo wanufaika na walengwa katika ngazi ya Mikoa na Halmashauri.

Aidha, Katambi amezitaka Halmashauri nchini kutekeleza.agizo la  Mhe. Rais Samia na sheria ya manunuzi inyoataka asilimia 30 ya zabuni kwenye Halmashauri zipewe kampuni za vijana. Amesisitiza ukaguzi utafanyika juu ya utekelezaji wake, hivyo mabaraza ya Madiwani yamehimizwa kuhakikisha makampuni ya vijana yanapewa tenda.

Awali, Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo, Prof.Jamal Katundu, alibainisha vigezo ilivyotumia Ofisi hiyo kwa kushirikiana na TAMISEMI, katika kuvipata vikundi vya Vijana hao kuwa ni; Vijana wenye Ulemavu kupitia vyuo na vikundi wenye ulemavu, 

Prof. Katundu amebainisha vigezo vingine kuwa ni;Vijana waliojiunga kwenye vikundi vinavyojihusisha na shuguli za kiuchumi katika fani husika, Vikundi vinavyorejesha mikopo kwa wakati katika Halmashauri zao; pamoja naVijana wenye utayari wa kufanya shughuli za kiuchumi, 

Kwa upande wake, Mkurugenzi Msaidizi, Idara ya Serikali za Mitaa kutoka TAMISEMI, Humphrey Mniachi, amesema ugawaji wa vifaa hivyo ni utekelezaji wa dhana ya ugatuaji madaraka. Hivyo, amesisitiza kuwa TAMISEMI itawasimamia Vijana hao ili wavitumie vifaa hivyo katika kuongeza tija katika uzalishaji wa bidhaa na ukuzaji mitaji.

Kwa nyakati Tofauti, baadhi Vikundi vya Vijana kutoka katika Halmashauri ya jiji la Dodoma na Halmashauri ya Bahi kwa niaba ya vijana waliopata vifaa hivyo ambao waliwawakilisha katika hafla hiyo, wamesema kuwa Wanaishuru Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Samia Suluhu Hassan kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu kwa jitihada wanazo fanya za kuwawezesha vijana kujiajiri hususani kupitia vifaa mtaji.