Jumamosi , 8th Mei , 2021

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan, amesema kuwa kitabu cha maisha ya Mzee Mwinyi,alichokizindua hii leo kinafundisha mambo mengi ikiwemo la binadamu kupendana na si vyema kumfanyia mtu ubaya sababu hauwezi kujua kesho atakuwa nani.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, samia Suluhu Hassan

Kauli hiyo ameitoa hii leo Mei 8, 2021, wakati wa uzinduzi wa kitabu cha Rais Mstaafu Mzee Ali Hassan Mwinyi, kinachoitwa Mzee Rukhsa, ambapo ndani ya kitabu hicho Mzee Mwinyi amemuelezea Waziri mmoja ambaye aliamua kumtimua kwenye moja ya nyumba alizokuwa akiishi na kisha kumnyima vifaa vyake vya ujenzi wa nyumba yake aliyokuwa akiijenga maeneo ya Mikocheni.

"Mzee Mwinyi anatufundisha umuhimu wa sisi binadamu hususani viongozi kupendana na kushirikiana, mwaka 1981 aliteuliwa kuwa Waziri wa Nchi, baada ya uteuzi huo alitakiwa kuhama nyumba ambayo ilipangiwa kukaa Waziri mwingine, Waziri mpya alikuja nyumbani na kumtaka aondoke haraka hata bila kumpa nafasi ya kuhamisha vitu vyake vya ujenzi Mzee Mwinyi aliondoka",ameeleza Rais samia

"Baada ya kuchaguliwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na kufanyiwa vitimbwi hivyo vyote Mzee Mwinyi, alimteua Waziri huyo  kwenye Baraza lake la Mawaziri, sasa ndugu zangu kama huyo Waziri bado anaishi sijui anajisikiaje huko aliko", ameongeza Rais Samia.