Alhamisi , 15th Jul , 2021

Baadhi ya wanawake waliohitimu vyuo vikuu nchini wamesema wanalazimika kuingia kwenye ndoa ili kujikwamua kiuchumi kutokana na kukosekana kwa ajira.

Picha: wahitimu wakifurahia jambo (Picha kutoka mtandaoni)

Akielezea kuhusu jambo hilo Tofana Paschal ambaye ni mmoja wa wanwake waliohitumu Chuo Kikuu amesema wanalazimika kuolewa ili kuweza kutimiziwa mahitaji ya kila siku tofauti na wakiwa nyumbani ambapo wanakuwa mizigo kwa wazazi wao.

“Tumelazimika kuolewa kwa lazima, unaona ni bora niende nikaishi na mwanaume kwa sabbau atapamabana ataleta kitu chochote kile nyumbani ilimradi tule tulale, imefika mahali wazazi nao wanachoka kuombwa kila kitu,” amesema Tofana.

Nao wadau wa elimu wamesema kuwa mfumo wa elimu Tanzania umekuwa ukitajwa kuwa si rafiki kwa maisha halisi ya mtaani hii ni kutokana na kuwepo kwa wimbi la wasomi wengi mtaani wasio na jaira.

Aidha, wadau hao wametoa wito kwa wanafunzi kuwa na machaguo sahihi wanapokwenda vyuoni ili wafanikiwe huku wakiiomba serikali kuyapa kipaumbele masomo ambayo yanaweza kumsaidia kijana kujiajiri pindi anapomaliza masomo.

“Wasomi wengi sana wako mtaani kwa kukosa ajira, ninaomba wanafunzi wawe makini na hizi taaluma wanazozichagua lakini pia serikali iongeze nguvu kwenye vyuo vya maendeleo na VETA ili tuweze kupata wataalamu zaidi,” amesema Emmanuel Ngelime.