Jumatatu , 7th Aug , 2017

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli ameendelea kuwaonya Watanzania wenye tabia ya uvivu na kupenda kubweteka bila kujituma, huku akisema wakati wa utawala wake hakutakuwa na vitu vya bure.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli.

Rais Magufuli ameyasema hayo leo alipokuwa akihutubia wananchi wa wilaya ya Korogwe mkoani Tanga waliohudhuria uzinduzi wa kituo cha mabasi (Stand) wilayani humo, na kusema kuwa watu wanaopenda kukaa vijiweni bila kujishugulisha huku wakilalamika njaa na hakuna pesa, ni bora wafe na njaa.

" Wakati wa kukaa kwenye magenge na kupiga maneno umepitwa na wakati, mnakaa kwenye pool unasubiri vitakuja hakuna, vya namna hiyo nataka kuwaeleza havitakuja kwenye utawala wangu, mnakaa mnasubiri tuna njaa tunataka mtuletee, mimi njaa nafuu ikuue kuliko nikuletee chakula, kwa sababu kama mwenzako ana chakula wewe una njaa, hatuwezi tukavumilia vitu vya namna hiyo", alisema Rais Magufuli.

Rais Magufuli aliendelea kusema ni lazima awaeleze Watanzania ukweli kuhusu hilo, bila kujali kuchukiwa kwani atasimamia haki huu akiwa na dhamira ya kwenda mbele.

"Ni lazima niwaeleze ukweli, nafuu mnichukie lakini niwaeleze ukweli, lakini hata mkinichukia hata sura yangu wala haipendezi, lakini mimi nitasimamia haki ya kuwaeleza ukweli, tunataka twende mbele, tunataka tubadilishe nchi, serikali itafanya juhudi zake zote kuwasaidia Watanzania", alisema Rais Magufuli