Jumanne , 22nd Jun , 2021

Katika tukio ambalo sio la kawaida kwa mila na tamaduni zetu, mzee wa miaka 80 aitwaje Khalid Segereje Mkazi wa kijiji cha Mwamgongo mkoani Kigoma amefikishwa katika Mahakama ya wilaya ya Kigoma na mtoto wake wa kumzaa ambaye anadai ampatie urithi wake.

Mzee Khalid Segereje (80), alipofika Mahakamani kwa ajili ya kusikiliza kesi aliyofunguliwa na mtoto wake

Mzee huyo amefikishwa Mahakamani hapo akifunguliwa shtaka la madai na mtoto wake aitwaye Abas Khalid kesi hiyo ya madai ya mirathi namba 8 ya mwaka 2021, ikiwa ni rufaa kutika Mahakama ya Mwanzo ya Kalinzi alipokuwa amefungua kesi hiyo awali na Mahakama hiyo kumpa ushindi mzee huyo hali iliyosababisha kijana wake kukata rufaa katika ngazi ya juu zaidi.

Kesi hiyo inasikilizwa na Hakimu Mfawidhi wa Mahakama hiyo Kenneth Mutembei ambaye aliutaka upande wa mlalamikaji ueleze kwa nini yuko Mahakamni hapo hatua iliyoleta kigugumizi kwake na baada ya Hakimu kumsihi kwa muda akaeleza kuwa amelazimika kufungua kesi hiyo dhidi ya baba yake mzazi kutokana na kutokunufaika na mali ambazo zilikuwa za baba yake na mama yake ambaye tayari ameshafariki dunia na mzee huyo kuoa mwanamke mwingine ambaye ndiye anayenufaika yeye na watoto wake.

Wakili upande wa utetezi Thomas Msasa ambaye ameeleza kujitolea kumsaidia mzee huyo akiongea mara baada ya maelezo ya shauri hilo kusikilizwa amesema anaamini atasimamia vyema kuhakikisha haki ya mzee haipotei.

Hakimu Mutembei baada ya kusikiliza maelezo ya shauri hilo akatoa uamzi wa shauri hilo kuendeshwa kwa njia ya maandishi hivyo upande wa mlalamikaji watatakiwa kuwasilisha hoja zao kwa maandishi ifikapo 28 Juni 28 mwaka huu na huku upande wa utetezi ukitakiwa kuwasilisha majibu mnamo Julai 5 kisha 12 Julai pande zote mbili zitafika Mahakamani hapo kwa ajili ya kupangiwa tarehe ya hukumu.