Ijumaa , 13th Oct , 2017

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga RPC Benedict Michael Wakulyamba, amethibitisha tukio la mtoto kuungua hadi kufariki kwa moto uliowashwa na mama yake kwaajiuli ya kupikia wilayani Handeni.

RPC Benedict amesema tukio hilo limetokea Oktoba 12 mwaka huu katika kijiji cha Kwamwenda Kata ya Mlorwa Wilaya ya Handeni ambapo mtoto Kessy Kamuje mwenye miaka 3 amefariki kwa kuungua moto akiwa shambani na mama yake mzazi.

“Ni kweli tukio limetokea jana ambapo mtoto Kessy aliungua kwa moto baada ya mama yake kumlaza kwenye kibanda cha nyasi shambani ambacho kilishika moto aliokuwa ameuwasha kwaajili ya kupikia”, amesema RPC Benedict.

Kamanda ameeleza kuwa mama wa mtoto Kessy alifika shambani kwaajili ya shughuli za kilimo ambapo alimlaza mtoto kwenye kibanda cha nyasi na akawasha moto kwaajili ya kupika kisha akaendelea na shughuli za kilimo ndipo Kibanda kikashika moto na kumuunguza hadi kufa mtoto Kessy.

Kwa upande mwingine RPC Benedict amesema madereva kumi wa mabasi waliokamatwa jana kwa kosa la kuendesha kwa mwendokasi kinyume na sheria za usalama barabarani wanarajia kufikishwa mahakamani leo kwaajili ya kujibu mashitaka yanayowakabili.

“Ni kweli tumewakamata madereva 10, baadhi yao wanaendesha mabasi ya abiria yaendayo mikoani, wengine daladala za hapa jijini kwa makosa ya kuendesha mwendokasi na leo watafikishwa mahakamani kujibu mashitaka yao”, amesema RPC Benedict.