Jumamosi , 19th Mei , 2018

Maaskofu wote 34 wa Kanisa Katoliki nchini Chile wamemuomba Kiongozi wa Kanisa Katoliki Duniani, Papa Francis aridhie kujiuzulu kwao kutokana na kashfa ya udhalilishaji kingono iliyolikumba Kanisa hilo nchini humo.

Maaskofu hao wanatuhumiwa kwa kuzuia uchunguzi wa kashfa ya ngono inayomuhusu Kasisi mmoja anayetuhumiwa kwa kumlawiti mtoto mdogo wa kiume.

Kashfa hiyo inamhusu Askofu Juan Barros ambaye anatuhumiwa kutumia wadhifa wake ndani ya Kanisa Katoliki kujaribu kuzuia uchunguzi dhidi ya tuhuma za udhalilishaji kingono zinazomkabili Kasisi Fernando Karadima.

Maaskofu hao wameomba msamaha kwa waathirika na Kanisa kwa ujumla kwa makosa hayo makubwa na uzembe. Hata hivyo mpaka sasa haijafahamika kama Papa Francis ameridhia ombi la Maaskofu hao kujiuzulu.