Jumatano , 25th Mei , 2022

Mahakama ya wilaya ya Iringa, imemhukumu kifungo cha miaka 30 jela Jofrey Mtokama (21), mkazi wa Kijiji cha Igluba mkoani Iringa baada ya kupatikana na hatia ya kumbaka mtoto wa miaka 9, huku Jamhuri ikipinga adhabu iliyotolewa ni ndogo ukilinganisha na ukubwa wa kosa.

Jofrey Mtokama, aliyehukumiwa miaka 30 jela

Akisoma hukumu hiyo, Hakimu Mkazi Mwandamizi Emmy Nsangalufu, amesema Mtokama mkazi wa wa Kijiji cha Igluba wilayani Iringa amehukumiwa kifungo cha miaka 30 jela na kulipa faini ya shilingi laki tano kwa kosa la kumbaka mtoto wa miaka 09.

Akisoma maelezo mbele ya Hakimu huyo, mwendesha mashtaka Alice Thomas, akisaidiana na Jackline Nungu, amesema kuwa mtuhumiwa huyo alitenda kosa mnamo tarehe Mei 13, 2021 katika kijiji cha Igluba wilayani Iringa, mkoa wa Iringa.

Amesema kuwa mhumiwa huyo ambaye  kazi yake ni  kuchunga Ng’ombe alienda nyumbani kwa mtoto huyo usiku baada ya kugundua kwamba wazazi wa mtoto huyo walikuwa kwenye sherehe ya pombe kijijini hapo na kumrubuni kwamba anaitwa na mama yake.

Thomas aliielezea Mahakama kwamba baada ya kufanikiwa kumdanganya mtoto alimpeleka sehemu na kumbaka na kumsababishia maumivu sehemu zake za siri na kutokomea porini baada ya wazazi wa mtoto kurudi toka kwenye sherehe, mtoto huyo alimwambia mama kilichotokea na alipomchunguza sehemu zake za siri hizo alikuta damu zinatoka.

Baada ya hapo zoezi la kumsaka kijana huyo lilipoanza usiku wa manane na kufanikiwa kumkata akiwa amejificha kichakana karibu na pori la kijiji na kumpeleka katika serikali ya kijiji na hatimaye kumpeleka polisi na kesi ikafunguliwa.