Ijumaa , 25th Mei , 2018

Mwanamke mmoja anayejulikana kwa jina la Rose Mary Magombola ambaye alikuwa muuguzi Mkuu msaidizi wa hospitali ya Mkuranga ameuawa na mtu aliyetajwa kuwa ni mume wake, na kisha mwili wake kufukiwa pembezoni mwa nyumba yao.

Akizungumza na wwww.eatv.tv Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Wilaya Steven Mwandambo, amesimulia jinsi tukio hilo lilivyokuwa mara baada ya kuingiwa na hofu kwa kutomuona kazini bila taarifa, na mpaka pale ilipobainika kuwa mume wake alimuua na kumfukia.

“Siku ya tar 21 Jumatatu hatukumuona dada Mary Magombolwa akiwa kazini sasa tulitaka kujua kwa nini kwa sababu sio kawaida yake kutokuja kazini bila taarifa, baadaye tukaona kwa sababu labda ya uchovu labda alichoka tukahisi labda baadaye anaweza akaja, tukalisahau siku ikapita, Jumann asubuhi tulipomkosa tena ikabidi tuanze utaratibu wa kutafuta nini kinaendelea, tuende nyumbani kwake kumuuliza mumewe kama amemuona au ana shida yoyote zaidi mpaka haonekani, lakini kabla hatutatoka hospitali, mume wake alifika na kutuuliza kama mke wake amefika kazini, sasa tulipata utata kidogo maana tulitegemea yeye ndio atupe majibu”, amesema Dk. Mwandambo.

Dk. Mwandambo ameendelea kwa kusema kwamba …... “sisi tukasema huku hajafika tangia jana na tulikuwa tunakuja kwako kukuuliza, kwa sababu na wewe hujui ni bora ukaenda polisi uende ukatoe tarifa, tukamsindikiza akatoa taarifa, na upelelezi ukaanizia pale kwa ajili yakumtafuta, na polisi wakafanya kazi, yeye mwenyewe akawekwa ndani kwa ajili ya kusaidia uchunguzi, na jana ndio ikajulikana kuwa alikuwa ameuawa na kufukiwa katika eneo la nyumba yake”.

Taarifa zaidi zinasema kwamba baada ya upelelezi wa kina mume wa nesi huyo ambaye jina lake halikuwekwa wazi kwa haraka, aliweka wazi kuwa amemuua mke wake na kumfukia karibu na eneo la nyumba yao.

Jeshi la Polisi lilifika eneo la tukio kufukua mwili wa nesi huyo, na kisha kwenda kufanyiwa uchunguzi na kutangazwa kuwa utazikwa mapema hii leo.