Alhamisi , 24th Mei , 2018

Chama cha Wananchi (CUF), kimesema kimeandika barua rasmi kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Magufuli ili kusaka muafaka wa kisiasa Visiwani Zanzibar.

Kauli hiyo ya CUF imetolewa leo Jijini Mwanza na Katibu Mkuu wa chama hicho, Maalim Seif Sharrif Hamad katika mahojiano maalum yaliyoratibiwa na Umoja wa Vilabu Vya Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC) na kurushwa na vituo mbalimbali vya redio na mitandao ya kijamii.

"Mpaka sasa Ikulu bado haijajibu barua hiyo. Licha ya kuwepo kwa miafaka zaidi ya minne kati ya CUF na Chama cha Mapinduzi (CCM), lakini kumekuwa hakuna utashi wa kisiasa katika kusaka muafaka wa moja kwa moja kuhusu tofauti za kisiasa huko Zanzibar", amesema Maalim Seif.

Maalim Seif amewahi kuhudumu katika nyadhifa mbalimbali Visiwani Zanzibar, ikiwemo ya Waziri wa Elimu kwenye serikali ya Hayati Mzee Aboud Jumbe, Waziri Kiiongozi kwenye serikali ya Mzee Ali Hassan Mwinyi na Makamu wa Kwanza wa Rais kwenye serikali ya Dkt. Ali Mohamed Shein awamu ya kwanza baada ya kufikiwa kwa makubaliano ya kuundwa serikali ya Umoja wa Kitaifa mnamo mwaka 2010.