Jumatano , 23rd Jun , 2021

Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, limetangaza donge nono la kiasi cha shilingi milioni mbili kwa mtu yeyote atakayetoa taarifa za kweli na kwa usiri mkubwa kwa jeshi hilo kuhusu mtu anayefanya uhalifu wa kutumia silaha, lengo likiwa ni kuhakikisha mkoa huo unabaki kuwa shwari.

Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam Muliro Jumanne.

Kauli hiyo imetolewa leo Juni 23, 2021, na Kamanda wa kanda hiyo Muliro Jumanne, wakati akizungumza kwenye kipindi cha Capital Radio, na kwamba siri ya mtoa taarifa itatunzwa na pesa hizo atapatiwa kwa siri bila kuzungushwa.

"Tumeamua kutangaza donge nono la zawadi ambazo tutawapatia kwa siri watakaotuletea taarifa za kweli zilizosahihi za kuwakamata katika mazingira yoyote watu wanaojihusisha na vitendo vya unyang'anyi wa kutumia silaha, na wakikamatwa pamoja na silaha zao, tutatoa milioni 2 palepale mchezo ukikamilika anapewa pesa yake hakuna mzunguko na hili ni zoezi endelevu," amesema Kamanda Muliro.

Aidha, Kamanda Muliro amewataka wahalifu Jijini Dar es Salaam kuchagua mambo mawili kuendelea kuingia kwenye msuguano na jeshi la polisi ama kuwa raia wema.