Alhamisi , 24th Mei , 2018

Mbunge wa Bunda mjini (CHADEMA) Ester Bulaya amesema Shirika la Umeme nchini (TANESCO) limefirisika kutokana na mzigo mkubwa wa madeni ambayo yanaongezeka kila baada ya mwaka na hivyo kupelekea shirika hilo kujiendesha kihasara.

Mbunge huyo amesema hayo leo Mei 24, 2018, Bungeni Jijini Dodoma wakati wa kuchangia hoja Wizara ya Nishati kwa mwaka wa fedha 2018/2019 na kusema kuwa kwa mujibu wa ripoti ya mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali deni hilo limeongezeka kwa asilimia 23 mpaka kufikia mwaka 2015.

Ukiangalia ripoti ya CAG imesema kabisa madeni hayana uwiano kati ya mali za shirika la TANESCO na madeni, kwa namna nyingine TANESCO imefirisika, hili shirika ni wakati muafaka sasa likagawanywa yakawa mashirika mawili likawa linadeal masula ya uendeshaji na uzalishaji, Dunia nzima inafanya (hivyo)” amesema Bulaya

Bulaya ameongeza kwamba kama serikali ina lengo la kujenga Tanzania ya viwanda basi viongozi wanapaswa kuandaa mipango mizuri ya uzalishaji na usambazaji wa umeme nchini.

Bunge kwa sasa linachangia hoja mjadala wa Wizara ya Nishati kwa mwaka wa fedha 2018/2019 na Waziri Dkt. Medadi Kalemani ameomba wabunge kuizinisha jumla ya shilingi trilioni 1.69 ambapo shilingi trilioni 1.66 kwa ajili ya miradi ya maendeleo na bilioni 27.1 kwa ajili ya matumizi ya kawaida.