Alhamisi , 21st Jul , 2022

klabu ya Azam FC imethibitisha kupona na kurejea uwanjani kwa winga wake hatari Iddi Seleman ‘Nado’ aliyekaa nje karibu msimu mzima uliomalizika akiuguza majeraha yake.

Iddi Seleman ‘Nado’

Nado aliumia goti la kulia Novemba 30, 2021 kwenye mechi ya ligi dhidi ya Mtibwa Sugar Azam ikishinda 1-0 nyumbani na baada ya hapo hakuonekana tena uwanjani akiicheza.

Baada ya kuumia alifanyiwa oparesheni ya tatizo alilolipata (Anterior Cruciate Ligament) na kutakiwa kukaa nje kwa miezi saba hadi tisa ili kupona kabisa.

Kurejea kwa Nado ni furaha kwa mashabiki wa timu hiyo kwani amerudi kipindi ambacho timu ndio imeanza maandalizi ya msimu ujao.

Tayari winga huyo anayesifika kwa kasi, chenga kufunga na kutengeneza mabao ameanza rasmi mazoezi na wenzake katika kambi inayoendelea kwenye viwanja vya Azam Complex Chamazi.

Nado atakuwa sehemu ya kikosi cha Azam kitakachosafiri Kesho kutwa Julai 22, 2022 kwenda nchini Misri katika mji wa El Gouna kuweka kambi kujifua na msimu ujao ambao itashiriki mashindano ya ndani na Kombe la Shirikisho Afrika.