Ijumaa , 14th Jul , 2017

Klabu ya Yanga kupitia Katibu Mkuu wake Charles Boniface Mkwasa leo wamemtangaza rasmi aliyekuwa Afisa habari wa Mbeya City Dismas Ten kuweza kuwatumikia wanayanga baada ya kuingia naye mkataba leo

Katibu Mkuu wa Yanga, Charles Boniface Mkwasa

Mkwasa amebainisha hayo kwenye mkutano wake na waandishi wa habari uliofanyika makao makuu ya klabu hiyo eneo la Jangwani Kariakoo Jijini Dar es Salaam ambapo Dismas anachukua nafasi iliyoachwa wazi na aliyekuwa Afisa Habari wa klabu hiyo Jerry Murro ambaye amemaliza kutumikia adhabu yake Julai 2 mwaka huu ya kutojihusisha na masuala ya mpira na Shirikisho la mpira wa Miguu Tanzania (TFF).

"Tumeamua kuleta mapinduzi kwenye utoaji habari kwenye klabu yetu na naamini kwa muunganiko huu wa Dismas na Chicharito klabu yetu itafanikiwa sana kupitia kitengo hiki cha habari na mawasiliano kama vilabu vingine vikubwa duniani", amesema Mkwasa.

Pamoja na hayo, Mkwasa amesema nafasi hiyo ilikuwa ikikaimiwa na Godlisten Anderson Chicharito kama kaimu afisa habari ambaye sasa ataendelea na nafasi hiyo chini ya Dismas Ten.

                            Afisa habari mpya wa yanga Dismas Ten (katikati) akiwa anaongea 

Kwa upande mwingine, Mkwasa amedai mwenyekiti wa klabu hiyo bado anaendelea na zoezi la usajili na mambo yakiwa mazuri ataweza kuweka bayana ni mchezaji gani mpya wamemnasa.