Ijumaa , 21st Apr , 2017

Shirikisho la mpira wa miguu Tanzania (TFF), limemfungulia mashtaka ya kinidhamu Msemaji wa Simba Bw. Hajji Manara kwenye Kamati ya Maadili

Mwesigwa (Kushoto) na Manara

Taarifa iliyotolewa na shirikisho hilo imesema kuwa Manara atapewa mashtaka yake leo na kujulishwa lini na wapi yatasikilizwa.

"Kwa mujibu wa Katiba ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), kila mwanafamilia wa mpira wa miguu Tanzania analazimika kuheshimu na kufuata kanuni za maadili za shirikisho kama zilivyoainishwa kwenye kanuni zake mbali mbali" Imesema sehemu ya taarifa hiyo.

Kuhusu aina za wanafamilia wa mpira nchini, taarifa hiyo imetaja kuwa wanafamilia wa mpira wa miguu ni pamoja na wachezaji, makocha, waamuzi, viongozi wa mpira wa ngazi zote na waajiriwa wa taasisi ambazo ni wanachama wa TFF wa ngazi mbalimbali.

Taarifa hiyo imesema kuwa TFF inaendelea kutoa rai kwa wadau wa mpira kuwa pamoja ni kwamba ni haki yao kushauri, kupendekeza, kukosoa lakini yote haya yafanyike kwa staha ili kutunza heshima ya mpira wetu.

Siku Jumanne wiki hii, Mkuu huyo wa Idara ya habari na Mawasiliano wa Simba, Haji Manara alizungumza na waandishi wa habari kuhusu sakata la pointi 3 za Simba na Kagera Sugar, ambapo aliishushia tuhuma nzito TFF hasa viongozi wake wakuu Jamal Malinzi na Celestine Mwesigwa kuwa lengo lao ni kuibeba Yanga na kuikandamiza Simba