Jumanne , 14th Nov , 2017

Kikosi cha timu ya taifa ya Tanzania Taifa Stars kimewasili nchini leo asubuhi kikitokea nchini Benin ambako kilienda kucheza mechi ya kirafiki ya kalenda ya FIFA.

Taifa Stars ilicheza dhidi ya Benin siku ya jumapili Novemba 12 ambapo mchezo huo ulimalizika kwa sare ya ba 1-1. Katika mchezo huo bao pekee la kusawazisha la Taifa Stars lilifungwa na Elias Maguli dakika 51 baada ya kupokea pasi ya Shiza Kichuya.

Kikosi hicho kamili kikiongozwa na benchi la ufundi chini ya kocha mkuu Salum Mayanga kimewasili asubuhi ya leo kwenye uwanja wa ndege wa kimataifa wa Mwalimu Nyerere na kupokelewa na viongozi wa shirikisho la soka nchini TFF.

Kurejea kwa Taifa Stars kunatoa mwanya kuanza kwa maandalizi ya timu za Kilimanjaro stars inayowakilisha Tanzania bara pamoja na Zanzibar Heroes ambayo inaiwakilisha Zanzibar katika michuano ya kombe la CECAFA Challenge inayoanza baadae mwezi ujao.