Jumapili , 16th Jul , 2017

Washindi wa Kombe la FA Simba SC, wanatarajia kuondoka nchini siku ya kesho (Jumatatu) alfajiri kuelekea Afrika Kusini kwa ajili ya kujiandaa michuano ya Ligi kuu inayotarajiwa kuanza mapema mwezi ujao kwa msimu wa mwaka 2017/2018.

Hayo yamewekwa wazi na taarifa iliyotolewa na Idara ya Habari na Mawasiliano ya klabu hiyo, ambapo imesema ikiwa Afrika ya Kusini itacheza mechi kadhaa za kujipima nguvu na vilabu vilivyopo huko kabla ya mchezo wake wa kwanza Agosti 8 mwaka huu (SIMBA DAY), utakaopigwa katika uwanja wa Taifa Jijini Dar es Salaam.

Pamoja na hayo, taarifa hiyo ilienda mbali zaidi na kusema wachezaji waliopo kwenye kikosi cha timu ya Taifa Stars hawataondoka siku ya kesho na badala yake wataendelea kubaki kwenye kambi ya Taifa Stars mpaka pale watakapomaliza mchezo wa marudiano dhidi ya Rwanda utakaochezwa mjini Kigali mnamo Julai 22 nchini Rwanda.

Wakati huo huo, klabu ya Simba imeungana na wanamichezo na watanzania wengine kumpa pole Waziri mwenye dhamana ya michezo nchini Dr Harrison Mwakyembe kwa kuondokewa na mke wake Bi. Linnah Mwakyembe.