Jumapili , 19th Nov , 2017

Kikosi cha vinara wa ligi kuu soka Tanzania bara Simba, kinarejea leo jijini Dar es salaam baada ya michezo yake miwili ya ligi kuu jijini Mbeya.

Taarifa iliyotolewa na klabu hiyo imesema kikosi kizima ambacho kilikuwa jijini Mbeya, kipo njiani hivi sasa kikirejea jijini Dar es salaam.

Simba ikiwa jijini Mbeya imefanikiwa kuibuka na alama sita katika michezo yake miwili ya raundi ya tisa na kumi. Mchezo wa raundi ya tisa Simba ilishinda bao 1-0 dhidi ya Mbeya City. Jana pia imefanikiwa kushinda bao 1-0 dhidi ya Tanzania Prisons.

Simba inaongoza ligi ikiwa na alama 22 baada ya michezo kumi ya ligi ikiwaacha wapinzani wao Yanga yenye alama 17 ikiwa na michezo 9. Azam FC yenye michezo 9 ina alama 19.